Ripoti ya Tume ya Rais ya Kuchunguza Ghasia za Uchaguzi wa 2025 imeweka wazi kuwa usalama wa taifa katika karne ya 21 umevuka mipaka ya matumizi ya silaha za moto na sasa unategemea zaidi usalama wa taarifa.
Kufuatia matukio ya ghasia yaliyochochewa na majukwaa ya kidijiti, Tume imesisitiza kuwa elimu ya kidijiti kwa wananchi si jambo la hiari tena, bali ni hitaji la lazima la kiusalama. Hii ni kutokana na ukweli kwamba taarifa potofu zinaweza kusambaa kwa sekunde chache na kuwafikia mamilioni ya watu bila kuchujwa, jambo linaloweza kuibua hasira na maamuzi ya kukurupuka yanayotishia utulivu wa nchi.
Moja ya mafunzo makubwa yaliyopatikana ni umuhimu wa kuwafundisha wananchi, hususan vijana ambao ndio watumiaji wakuu wa mitandao, namna ya kuthibitisha ukweli wa picha na habari kabla ya kuzisambaza.
Ripoti imebainisha kuwa mbinu za kisasa kama matumizi ya picha zilizochezewa (deepfakes) na Akili Unde (AI) zilitumika kama silaha za kisaikolojia kuaminisha umma uongo, kama vile uwepo wa makaburi ya halaiki. Hivyo, uwezo wa mwananchi mmoja mmoja kuchambua taarifa unatajwa kuwa ndio kinga ya kwanza dhidi ya propaganda zinazolenga kuibua vurugu na kuharibu miundombinu muhimu ya nchi.
Aidha, ujenzi wa utamaduni wa mazungumzo yenye staha mtandaoni umeelezwa kuwa nguzo muhimu ya mshikamano.
Tume ilibaini kuwa lugha za chuki, kejeli, na kaulimbiu za uchochezi zilizosambaa kwenye majukwaa ya WhatsApp, X, na TikTok zilichangia kwa kiasi kikubwa kuhamishia uhasama kutoka kwenye ulimwengu wa kidijiti kwenda kwenye maisha halisi.
Ili kuzuia hali hii isijirudie, kuna haja ya kuimarisha mifumo ya mamlaka kama TCRA katika kufuatilia viashiria vya hatari mapema, huku jamii ikihimizwa kutumia teknolojia kwa ajili ya maendeleo badala ya kuibomoa nchi.
Aidha ripoti imesema kuwa amani ya Tanzania itategemea uwajibikaji wa kila mtumiaji wa mtandao. Kila mwananchi anapaswa kutambua kuwa kila picha au ujumbe anaosambaza unaweza kuwa na athari kubwa kwa usalama wa taifa na utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya 2050.
Katika dunia inayozidi kuwa ya kidijiti, kulinda ukweli na maadili ya mawasiliano ndiyo njia pekee ya kuhakikisha kuwa teknolojia inabaki kuwa chombo cha kukuza demokrasia na kuimarisha umoja, badala ya kuwa chanzo cha maangamizi na migogoro ya kijamii.
@@@@@@@@@@
SERIKALI YAHIMIZA ULINZI WA AMANI KAMA NGAO YA MAENDELEO YA TAIFA
Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, amewahimiza Watanzania kulinda na kutunza amani kwa wivu mkubwa ili kuwezesha nchi kufikia malengo yake ya kimaendeleo.
Akizungumza na waandishi pamoja na maofisa habari mkoani Njombe, Msigwa alisisitiza kuwa hakuna nchi duniani iliyowahi kupata maendeleo ya kweli ikiwa wananchi wake wanavurugana na kugombana kila kukicha.
Alieleza kuwa ni jukumu la kila mwananchi kukataa hamasa zozote zinazoashiria fujo na vurugu, akionya kuwa mabeberu bado hawajalala na mara nyingi hutumia baadhi ya Watanzania miongoni mwetu kufanikisha ajenda zao za kuvuruga nchi.
Msigwa alifafanua kuwa ni vigumu kupiga hatua za kiuchumi ikiwa jamii itajikita kwenye maandamano ya kila siku na uharibifu wa miundombinu ambayo ndiyo uti wa mgongo wa biashara na usafirishaji.
Alitolea mfano wa wakulima wa maparachichi mkoani Njombe ambao wanategemea utulivu ili kuzalisha, akibainisha kuwa vitendo vya kuchoma bandari au viwanja vya ndege vinavyohamasishwa na baadhi ya watu kwenye mitandao ya kijamii vitaathiri uwezo wa kusafirisha bidhaa hizo kwenda nje ya nchi.
Aliongeza kuwa uharibifu wa mali za umma, kama mabasi ya mwendokasi, unamuumiza mwananchi wa kawaida ambaye kesho yake atakosa usafiri wa kumuwezesha kufanya kazi zake za kila siku.
Katika kulinganisha na hali ya kimataifa, Msemaji huyo wa Serikali alikumbusha madhara makubwa ya vita yanayoendelea katika nchi za Israel na Iran, akieleza namna mataifa hayo yanavyorudi nyuma kimaendeleo kutokana na ukosefu wa utulivu.
Aliwataka maofisa habari nchini kote kuendelea kuwaelimisha na kuwahamasisha wananchi juu ya umuhimu wa kudumisha mshikamano. Alisisitiza kuwa utulivu wa nchi ndio msingi pekee utakaowezesha utekelezaji wa ndoto kubwa za Dira ya Maendeleo ya mwaka 2050 kwa maslahi ya kizazi cha sasa na kijacho.
@@@@@@@@@@@
MCONGO AWAONYA WATANZANIA KUACHA UJINGA WA KUCHEZEA AMANI MITANDAONI
Raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Ability Sweli, ambaye anaishi nchini Tanzania kwa shughuli za utafutaji maisha, ametoa onyo kali kwa Watanzania wanaotumia mitandao ya kijamii kuchochea uvunjifu wa amani, akieleza kuwa vitendo hivyo ni vya kijinga na vinaweza kuliingiza taifa katika majanga makubwa.
Sweli ametoa kauli hiyo kufuatia kuongezeka kwa mahimizano ya vurugu yanayofanywa na baadhi ya watu mtandaoni, akisisitiza kuwa yeye ni mwathirika wa moja kwa moja wa vita nchini kwake na ameshuhudia kwa macho yake namna machafuko yanavyoweza kuporomosha maisha ya mtu mmoja mmoja na uchumi wa nchi kwa ujumla ndani ya muda mfupi.
Akizungumzia uzoefu wake wa kuishi kwenye mazingira ya kivita nchini Kongo, Sweli amebainisha kuwa vita si jambo la kusimuliwa wala kufanyiwa majaribio, kwani huondoa hali ya utulivu na kusitisha maendeleo yote ya kijamii na kiuchumi.
Ameeleza kuwa mnyororo wa maendeleo unategemea amani, na kwamba pasipo amani hakuna mwananchi anayeweza kufanya shughuli zake kwa uhuru wala kupanga mipango ya baadaye. Sweli ametolea mfano wa Soko la Kariakoo jijini Dar es Salaam, akisema kuwa soko hilo limekuwa kivutio cha wafanyabiashara kutoka mataifa mbalimbali kutokana na utulivu uliopo nchini, jambo ambalo amedai kuwa ni nadra kuliona katika maeneo yenye migogoro nchini kwake DRC.
Mwathirika huyo amefafanua kuwa wengi wa wanaohamasisha vurugu na kuvunja amani mitandaoni hufanya hivyo kwa sababu hawajawahi kuishi kwenye mazingira ya vita, hivyo hawawezi kutambua thamani ya neema waliyonayo kwa sasa.
Ameonya kuwa siku ambayo vita itatokea na kuwalazimu kuishi ndani ya milio ya risasi, ndipo watakapogundua kwanini kuna umuhimu wa kuhimiza amani kila siku na kwanini sauti za wanaopigania utulivu zinapaswa kuheshimiwa.
Kwa mujibu wa Sweli, faida ya amani huonekana zaidi baada ya watu kupoteza kila kitu kutokana na vita, hali ambayo amewaomba Watanzania wasiiruhusu iwafikie kwa kufuata ushauri wa kijinga unaosambazwa katika majukwaa ya kidijitali.
Aidha, amewataka wananchi kuzingatia amani waliyonayo kama kipaumbele namba moja, akisisitiza kuwa uhuru wa kufanya biashara, kutembea na kujenga nchi unategemea usalama wa mipaka na mioyo ya watu.
Sweli ambaye anaishi nchini kwa mujibu wa taratibu na sheria za uhamiaji, amesema kuwa uzoefu wake wa kuporomoka kimaisha wakati wa vita nchini mwaka unatosha kuwa fundisho kwa yeyote anayedhani kuwa vita ni suluhisho la changamoto za kijamii.
Amesisitiza kuwa ni wakati wa Watanzania kupuuza kila aina ya uchochezi wa mtandaoni na badala yake waendelee kuilinda tunu ya amani ambayo ndiyo siri ya maendeleo makubwa ya kiundombinu na kibiashara yanayoonekana nchini kwa sasa
