Read more
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amewahakikishia
wakazi wa mji mdogo wa Katesh walioathirika na mafuriko makubwa kuwa serikali itarejesha
huduma zote za msingi za kijamii.
Rais Samia amesisitiza kuwa serikali itaendelea kufanya tathmini ya uharibifu wa mali huku
akiiagiza Wizara ya Nishati kuangalia uwezekano wa upatikanaji wa umeme wa dharura
baada ya miundombinu kuharibika na maafa haya ili shughuli za uopoaji zifanyike usiku na
mchana.
Rais Samia ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wananchi na waathirika mara baada
ya kutembelea maeneo yaliyoathirika na mafuriko hayo na kushuhudia hali halisi ya uharibifu
wa maafa.
Aidha Rais Samia ameongeza kuwa mbali na michango mbalimbali iliyotolewa ndani ya nchi
lakini pia kumetolewa takriban Shilingi bilioni 2.5 kutoka kwa wahisani walioshiriki kwenye
mkutano wa COP 28, Dubai.
Miongoni mwa maeneo aliyotembelea Rais Samia ni Hospitali ya Tumaini wilayani humo
kwa ajili ya kuwajulia hali na kuwafariji majeruhi na pia shule ya Sekondari ya Katesh
ambapo ndipo makazi ya muda yalipowekwa ili kuwastiri waathirika hao.
Vile vile, Rais Samia ametaka tahadhari zote za msingi zichukuliwe ili kusitokee janga
jingine la mlipuko wa magonjwa hivyo kuheshimu kanuni za usafi kwani amesema majanga
wakati mwengine huzua maradhi kama kipindupindu.
Hivyo Rais Samia ameielekeza Wizara ya Maji kuhakikisha huduma za maji safi na salama
zinaendelea kupatikana muda wote huu hususan maeneo yaliowekwa makambi ya kustiri
waathirika wa janga hilo.
Mafuriko mazito yaliotokea yamesababisha vifo vya Watanzania 76 hadi sasa, huku kaya
1,150 zikiwa zimeathirika na watu 5,600. Pia kumekuwa na majeruhi zaidi ya 117 pamoja na
uharibifu wa miundombinu ya barabara, maji na umeme.




0 Reviews